Serikali imesaini mkataba wa
makubaliano ya ushirikiano na nchi ya Singapore kwa ajili ya uboreshaji
mipango miji Lindi,Mtwara,Dar es Salaam na Arusha
Akizungumza baada ya utiaji saini huo jana, Katibu
Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Kidala
alitolea mfano wa Dar es Salaam kuwa, tangu miaka ya 1990 mpango wa
uboreshaji jiji haujabadilishwa.
“Kutokana na mkataba huu, sasa mpango wa
uboreshaji Jiji la Dar es Salaam na majiji mengine utapitiwa na
kufanyiwa marekebisho yanayoendana na wakati huu,” alisema Kidala na
kuongeza;
“Kuna kampuni kutoka nchini Italia ambayo imeandaa
uboreshaji huo, utapitiwa na Shirika la Upangaji Miji la Singapore
kabla ya kuanza utekelezaji.”
Alisema mkataba huo umelenga maeneo matatu ambayo
ni; uboreshaji mipango miji, ushirikiano wa ujenzi nyumba za gharama
nafuu na kujenga mfumo mzuri wa kumiliki ardhi.
Naye Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya
Makazi, Goodluck Ole-Medeye alisema makubaliano hayo yametokana na
ziara iliyofanywa hivi karibuni nchini Singapore na Rais Jakaya Kikwete
na wabunge wa Kamati ya Bunge ya Bajeti na Hesabu za Serikali (PAC).
“Mikoa ya Lindi na Mtwara kuna shughuli za
uchumbaji gesi, hivyo ni muhimu kuhakikisha uendelezaji majengo na
miundombinu ya eneo hilo inakuwa ya kisasa,” alisema Medeye na kuongeza:
“Baadaye mpango huu utaendelea Mbeya, Mwanza na
Tanga. Singapore wamepiga hatua katika suala la uendelezaji miji, wana
uzoefu wa kutosha hivyo tunaamini watatusaidia.”
Alisema mpango huo umeanza rasmi jana kwa
wataalamu wa Tanzania kukutana na wale wa Singapore, kujadiliana mambo
ambayo wataanza kuyatekeleza katika mikoa na majiji hayo.
“Kuna masuala ya ardhi, nyumba na mengine mengi,
kila eneo lina wataalamu wake, kazi hii inaanza mara moja na itakuwa ni
ya miaka mitano,” alisema.
Mwenyekiti wa Shirika la Upangaji Miji la
Singapore, Seah Moon Ming alisema njia nzuri ya kuendeleza miji, ni kuwa
na mipango thabiti ya ujenzi mzuri wa nyumba na miundombinu.
Ming alisema licha ya kuendeleza miji, nchi yake
imetoa wataalamu ambao watashirikiana na wenyeji lengo likiwa ni kupiga
hatua kwenye maendeleo haraka, kwa wananchi kumudu gharama za nyumba
nafuu.
itakuwa vizuri
ReplyDelete