Mwishoni mwa wiki iliyopita, wezi walivamia na kuiba nyaya katika kituo cha kusambazia umeme cha Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Ubungo, Dar es Salaam hivyo kuathiri huduma ya umeme katika sehemu kubwa ya jiji hilo kwa takriban siku tatu.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Felchesmi Mramba, wizi huo umelisababishia shirika lake hasara ya Sh200 milioni.
Wakati hali ikiwa haijatengamaa, wezi tena
wameripotiwa kuiba vyuma vinavyobeba nyaya za umeme huko Kahama na
kusababisha sehemu kubwa ya wilaya hiyo hususan machimbo ya dhahabu ya
Bulyanhulu kukosa huduma ya nishati. Tanesco imesema wizi huo umelitia
hasara shirika hilo ya Sh1.2 bilioni.
Wizi katika miundombinu ya Tanesco siyo jambo
geni, tumekuwa tukisikia taarifa mbalimbali za tatizo hilo lakini
kimsingi hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa hazilingani na ukubwa wake.
Mathalan, akizungumzia wizi huu wa Ubungo, Mramba
alisema walinzi waliokuwa zamu katika kituo hicho wamekamatwa huku
akisema sehemu hiyo inakuwa ngumu kudhibiti wizi kutokana na mwingiliano
wa watu. Tunasema hapana. Hasara ya Sh200 milioni haiwezi kuishia kwa
walinzi kukamatwa, tunadhani hatua kubwa zaidi zinastahili kuchukuliwa
ili siyo tu tabia hiyo isijirudie tena katika maeneo hayo, bali iwe
funzo kwa wengine.
Tunaamini kabisa wapo watu waliopewa dhamana ya
kusimamia maeneo husika ulipotokea wizi huo, tungependa kusikia hatua
zilizochukuliwa dhidi yao.
Tanesco imekuwa ikilalamikia kutokuwa na fedha za
kutosha kukidhi mahitaji ya wateja wake ilionao sasa huku kukiwa na
foleni ndefu ya wengine wanaohitaji huduma hiyo nyeti ya nishati.
Hasara kama hii ikichangiwa na kuvuta miguu katika
kukusanya madeni, vimeilazimu kubeba magunia ya lawama. Kama
ilivyoeleza jana, Tanesco inazidai taasisi za Serikali kiasi cha Sh129
bilioni, kati ya hizo Sh70 bilioni zikiwa deni la Zanzibar.
Aidha, linawadai wateja binafsi pamoja na kampuni
mbalimbali kiasi cha Sh104 bilioni. Inasikitisha kwamba Tanesco imekuwa
ikitoa takwimu hizi za madeni hadharani lakini ufuatiliaji wake umekuwa
hafifu na dhaifu.
Katika hali ya kawaida, Serikali au taasisi zake
hazikupaswa kuwa katika mkumbo huu. Tunasema hivyo kwa sababu kila mwaka
fedha kwa ajili ya malipo ya huduma hiyo hutengwa na kupitishwa na
Bunge katika Bajeti, vinginevyo tuelezwe kwamba fedha hizo zimetumika
kwa ajili ya shughuli gani nyingine.
Pia Tanesco imeonyesha udhaifu mkubwa katika
ufuatiliaji wa madeni kwa watu binafsi na kampuni. Tungependa kusikia
hatua stahiki zikichukuliwa na shirika hilo dhidi ya wadaiwa sugu.
Sambamba na kuchukua hatua, tunadhani kwamba ipo
haja kwa Tanesco kuimarisha kitengo chake cha elimu kama ilivyo katika
baadhi ya taasisi za Serikali na mashirika mengine, ili kuwafanya wateja
wake kutoa ushirikiano na kuliwezesha kutimiza wajibu wake kwa jamii.
Kwa mfano, sababu zilizotolewa za wizi wa Kahama kwamba wezi
hutumia vyuma hivyo vyenye thamani kubwa kwa ajili ya kutengenezea
majembe, matoroli na kuviuza kama chuma chakavu, zingeweza kudhibitiwa
pia kwa kutoa elimu kwa wananchi.
Pamoja na mikakati ya maboresho inayoendelea hivi
sasa ndani ya shirika, tunautaka uongozi mpya wa Tanesco kuvalia njuga
matatizo hayo ambayo yanaonekana kuwa sugu vinginevyo itakuwa ndoto
kwake kupiga hatua za maendeleo. Kwa lugha za kisiasa, tunadhani umefika
wakati kwa Tanesco kujivua gamba ili kuleta matumaini ya kuiangaza
Tanzania kiuchumi.
0 comments:
Post a Comment