Kauli ya Rais Jakaya Kikwete ya kuwataka wanachama, wadau na makada wa CCM, kuondokana na unyonge, imepokewa kwa hisia tofauti huku ikielezwa kuwa ni ya vitisho.
Juzi, wakati akifungua Mkutano wa Halmashauri Kuu
ya CCM mjini Dodoma, Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa chama
hicho tawala alisema: “Ni wakati wa kuacha unyonge na uvumilivu una
kikomo chake.”
Alisema CCM inaingia kwenye uchaguzi huku
ikishindana na wagomvi: “...Ugomvi ndiyo sehemu ya mwongozo wao kufanya
siasa,” alisema Kikwete bila kutaja jina la chama chochote cha siasa.
Alisema amechoshwa na vitendo vya ugomvi huku
akitolea mfano wa tukio la Kahama mkoani Shinyanga ambako kijana mmoja
alitolewa macho kwa bisibisi na mwingine kumwagiwa tindikali katika
uchaguzi mdogo wa ubunge Igunga, mkoani Tabora.
Akizungumza kwa simu jana, Mwenyekiti wa Chadema,
Freeman Mbowe alieleza kushangazwa kwake na kauli ya Rais Kikwete
akisema: “Nimeipokea kwa mshtuko na ninawataka wafuasi wa chama changu
kuwa watulivu na kuchukua tahadhari kubwa.”
“Nilichokifanya ni kuwaagiza wafuasi wa Chadema
kufanya kampeni za kistaarabu kwa kutolipiza kisasi ili kuhakikisha
kwamba hakuna damu ya Mtanzania itakayomwagika Kalenga,” alisema.
Hatua ya Rais Kikwete, imekuja baada ya CCM
kumtangaza, Godfrey Mgimwa kuwa mgombea ubunge wa Jimbo la Kalenga.
Mgimwa ni mtoto wa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, ambaye pia alikuwa
Waziri wa Fedha, hayati Dk William Mgimwa aliyefariki mwezi uliopita
nchini Afrika Kusini.
Mgombea huyo atachuana na mgombea wa Chadema, Grace Tengega.
Jana, Mbowe alisema ingawa Kikwete ni Mwenyekiti
wa CCM, alitakiwa kufahamu kwamba ni kiongozi wa nchi na ni Amiri Jeshi
Mkuu ambaye vikosi vya Ulinzi na Usalama vipo chini yake.
“Anapotoa kauli nzito kama hiyo, inatakiwa afahamu
kwamba yeye si Mwenyekiti wa CCM tu, bali ni Rais na Amiri Jeshi Mkuu,
hakustahili kutoa kauli kama hiyo inayoweza kuamsha hisia,” alisema
Mbowe.
Alisema kauli zake za kiitikadi za kupendelea
chama chake wakati akifahamu kuwa yeye ni kiongozi wa Watanzania wote,
zinawafanya wananchi wagawanyike kwa misingi ya vyama.
“Rais Kikwete anadai kwamba mtu wao alimwagiwa
tindikali na mwingine kutolewa macho kwa bisibisi, lakini hazungumzii
viongozi na wanachama wa Chadema waliouawa kwa kupigwa risasi na wengine
kwa mabomu. Anasema hayo huku akifahamu fika kwamba kuna vyombo vya
dola na Mahakama ambavyo vinashughulikia matukio hayo.”
Mbowe alidai kuwa Juni 15, 2013 wakati akifunga kampeni za
udiwani mkoani Arusha, alirushiwa bomu la kivita na kusababisha vifo vya
watu wanne lakini uongozi wa chama hicho ulipomwomba Rais aunde tume
huru ya kimahakama hakuna kilichofanyika.
“Tumemwomba mara kadhaa Rais Kikwete kuunda tume
huru ya kimahakama ili kuchunguza mauaji ya viongozi na wanachama wa
Chadema ambayo yamekuwa yakitokea, lakini hakuna kilichofanyika,”
alisema Mbowe ambaye ni pia kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.
Alisema: “Rais Kikwete anasema wamekubaliana
kwenye Halmashauri Kuu (ya CCM) kuacha unyonge, Halmashauri Kuu ina
viongozi wote wakuu wa nchi, wanakubaliana kuwatenga wananchi kwa
kufuata itikadi za chama chao, hii ni hatari.”
Mbowe alisema kauli ya Rais Kikwete inafanana na
ile ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyoitoa bungeni ya kuwataka askari
polisi kuwapiga raia kwa wale wasiotaka kutii amri halali.
Akizungumzia kauli hiyo, Mwenyekiti wa Kituo cha
Demokrasia Tanzania (TCD), James Mbatia alisema ameshtushwa na kauli ya
Rais Kikwete na kumtaka kuitolea ufafanuzi ili kuondoa mgawanyiko katika
jamii.
Alisema kauli ya ‘unyonge CCM sasa basi’
haikupaswa kutolewa naye hasa ikizingatiwa kwamba ndiye kiongozi mkuu wa
nchi ambaye vyombo vya ulinzi na usalama viko chini yake.
“Ni kama amevielekeza vyombo vya ulinzi na usalama
kuchukua hatua kali dhidi ya vyama vingine vya siasa, ninamwomba
alitolee ufafanuzi suala hili kabla halijaleta madhara kwenye jamii,”
alisema Mbatia.
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alisema
kauli ya Kikwete inaashiria kuwa kutakuwa na matumizi makubwa ya vyombo
vya dola katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Kalenga.
“Ninavyofahamu siyo kwamba anawaagiza wafuasi wa
CCM kuacha unyonge na kuchukua hatua, bali anavielekeza vyombo vya dola
kutumia nguvu kubwa zaidi,” alidai.
Mtatiro alisema anashangaa kauli ya namna hiyo kutolewa na Rais wakati ndiye anayetakiwa kuhubiri amani na kuvumiliana.
Akizungumza suala hilo, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam, Bashiru Ali alisema wananchi wanatakiwa kuwa makini na kauli za
wanasiasa zenye kujenga chuki.
“Vijana tusipigane kwa kugombanishwa na wanasiasa,
tofauti zetu za kiitikadi zisitufanye tugombane kwani malengo ya
wanasiasa ni kutoa kauli zenye utata kwa lengo la kupata kura, matatizo
yetu yatuunganishe,” alisema Bashiru.
0 comments:
Post a Comment