Rais
wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Mwai Kibaki anatarajia kuwasili nchini tarehe
20 Februari, 2013 kwa ziara ya kitaifa ya siku mbili. Ziara hiyo ya Mhe.
Rais Kibaki inafuatia mwaliko wa Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Aidha, ziara ya Mhe. Rais Kibaki
inafanyika kufuatia ziara ya Mhe. Rais Kikwete nchini Kenya mwezi
Septemba, 2012.
Mhe.
Rais Kibaki ambaye anatarajiwa kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Julius Nyerere tarehe 20 Februari, 2013 saa 9.00 alasiri,
atapokelewa na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete.
Akiwa hapa
nchini, Mhe. Rais Kibaki atafanya mazungumzo rasmi na Mhe. Rais Kikwete
tarehe 20 Februari 2013 kabla ya kushiriki katika Dhifa ya Kitaifa
itakayoandaliwa kwa heshima yake na Mhe. Rais Kikwete, Ikulu, Dar es
Salaam.
Mhe.
Rais Kibaki anatarajiwa pia kukutana na Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam
tarehe 21 Februari, 2013, kuzindua Barabara ya Mwai Kibaki na kutembelea
Gereza Kuu la Ukonga Jijini Dar es Salaam ili kujionea shughuli
mbalimbali zinazolenga kuwarekebisha Wafungwa kuwa Raia wema na kuwapa
mafunzo ya kiufundi kuwawezesha kujitegemea wanapomaliza vifungo vyao.
Shughuli hizo ni pamoja na ushonaji, useremala na kilimo cha kisasa.
Mhe. Rais Kibaki ataondoka nchini tarehe 21 Februari, 2013 kurejea nchini kwake.
IMETOLEWA NA: WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA, DAR ES SALAAM.
19 FEBRUARI, 2013
0 comments:
Post a Comment