Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema,
Profesa Mwesiga Baregu amewataka viongozi wa chama hicho kutafakari na
kudhibiti madhara yanayoweza kukikumba hasa baada ya hatua yake ya hivi
karibuni ya kumvua nyadhifa zote, Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe na
wenzake wawili.
“Bahati nzuri wamevuliwa uongozi siyo uanachama,
binafsi nadhani viongozi wanatakiwa kutafakari na kudhibiti madhara
zaidi kwa chama, wakishupaza shingo, lolote litakalotokea watakuwa ni
sehemu ya lawama,” Profesa Baregu alisema Dar es Salaam jana.
Zitto, aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk Kitila
Mkumbo pamoja na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema mkoani Arusha, Samson
Mwigamba walivuliwa uongozi Novemba 22 mwaka huu, kwa tuhuma za kuandaa
waraka wa Mkakati wa Mabadiliko 2013, uliolenga kufanya mabadiliko
makubwa ya kiuongozi wakati wa uchaguzi mkuu wa ndani wa chama hicho
kinyume na katiba, sheria na itifaki za chama.
Profesa Baregu alisema pamoja na viongozi hao
kuvuliwa madaraka, mema waliyokifanyia chama hicho hayawezi kuyeyuka na
kwamba makosa yao yasikuzwe kiasi cha kufuta mazuri yao katika kujenga
chama hicho.
“Ni vigumu kuamini kwamba makosa ya Zitto, Dk
Kitila na Samson Mwigamba yanaweza kuyeyusha mema waliyokifanyia chama
kama barafu inavyoyeyuka juani.”
Profesa Baregu ambaye alikuwapo katika kikao
kilichowavua uongozi Zitto na wenzake alisema kinachotakiwa kufanyika
sasa ni kujenga uhusiano ndani ya chama na hasa kipindi hiki cha mpito
kuelekea uchaguzi mkuu wa ndani ambao umeanza Novemba 22 na unatarajiwa
kumalizika Juni mwakani.
Alitaka hatua dhidi yao zizingatie Katiba ya chama
hicho ili kuhakikisha kuwa hazivurugwi na mamlaka nyingine zilizopo
ndani ya Chadema akisema mkutano wa Baraza Kuu unaweza kubadili uamuzi
wa Kamati Kuu.
“Kinachotakiwa kufanywa ni kuwatangazia wanachama
misingi, taratibu na kanuni za kuzingatia katika harakati zao ili
kuondoa hali ya watu kufanya mambo kwa kificho,” alisema na kuongeza:
“Ni wazi wengi wapo katika kampeni, ichukuliwe
kuwa walioshughulikiwa wamebambwa na iwe njia ya kuonyesha ukomavu
katika kustahamiliana.”
Alisema asingependa kuona siasa za kulipizana
visasi na kusisitiza kwamba hata kama mwanachama ana chuki binafsi na
mwenzake, hatakiwi kutumia chuki hiyo kumhukumu.
“Tuhuma zinazotolewa dhidi ya Zitto na wenzake
kwamba wamenunuliwa na chama fulani cha siasa zinahitaji maelezo na
vielelezo vya kina ili kuwaaminisha wengi. Nasema hivi kwa sababu
historia yao inadhihirisha kuwa wana uchungu na chama chao. Chama
kinachoongozwa kwa demokrasia na kinachotarajiwa kushika madaraka ya
kuongoza nchi, lazima kionyeshe uwezo mkubwa wa kuvumiliana, kutafakari,
kusamehe, kuaminiana na kujenga umoja wenye lengo la kuelekea kusudio
lake.”
Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare
alisema chama hicho kipo imara na hakiwezi kuyumba kwa sababu ya uamuzi
huo.
Lwakatale ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya
chama hicho alisema: “Mfumo wa ulinzi ndani ya chama upo imara,
yakitolewa maelezo na ngazi za juu kinachofuata baada ya hapo ni
utekelezaji.”
Alisema kilichotokea ni kitu cha kawaida na ni mwanzo wa chama kujiimarisha.
Baadhi ya wajumbe wa Mkutano Mkuu na Baraza Kuu la
Chadema hicho Wilaya ya Temeke wamepinga hatua iliyochukuliwa na Kamati
Kuu ya kuwavua nyadhifa viongozi hao.
Mwenyekiti wa Vijana Mkoa wa Temeke, ambaye pia ni
Mjumbe wa Baraza Kuu na Mkutano Mkuu, Joseph Patrick aliwaambia
waandishi wa habari jana kuwa mgogoro huo haulengi kujenga chama, bali
unakibomoa.
“Chama chetu kimekuwa na tabia ya kuingia kwenye
migogoro kila panapokaribia uchaguzi wa ndani. Hii inasababisha
kuchafuana na kutukanana miongoni mwetu kiasi cha kuitana wahaini,
wasaliti na wengine kuwaita wenzao wanatumika kwa lengo la kuwadhoofisha
mbele ya wanachama,” alisema na kuongheza:
“Tumeona mifano mingi ya namna hii. Wakati Chacha
Wangwe akiwa hai alipotangaza kuwania uenyekiti, mgogoro wa namna hii
ulijitokeza, aliitwa majina yote na hakuwahi kusemwa vizuri kwenye
chama, hakuchafuliwa na watu walio nje ya chama, bali viongozi wenzake
waliotofautiana kimsimamo.”
Alisema hali hiyo ilijitokeza pia kwa Zitto
alipotangaza kuwania uenyekiti kama ilivyokuwa wakati wa chaguzi za viti
maalumu na mabaraza ya chama.
Alisema ni vyema viongozi wakaitisha mkutano mkuu
wa dharura na kuwaeleza wanachama mambo mbalimbali ikiwamo ni kwa nini
wameamua kusambaza waraka ambao alisema unakidhalilisha chama badala ya
waliouandika.
Katibu wa Chadema Mkoa wa Dar es Salaam, Herry
Kilewo amehojiwa na Polisi kwa kile kilichodaiwa kuwa ni kutokana na
madai ya Zitto kutishiwa kuuawa.
Katika mahojiano hayo, Kilewo aliongozwa na Mwanasheria wake,
Mussa Mfinanga, Mwanasheria wa Chadema John Malya na pia alikuwapo
Diwani wa Ubungo, Boniface Jacob. Mfinanga alisema Novemba 11 mwaka huu,
chombo kimoja cha habari kiliripoti kuwa Zitto ametishiwa kuuawa na
mteja wake Kilewo.
Mfinanga alisema baada ya madai hayo, Jeshi hilo
lilimwita Zitto kutoa maelezo yake na kisha kuona haja ya kumhoji Kilewo
shutuma hizo. Alisema mteja wake amejidhanini mwenyewe na yupo nje kwa
dhamana bila ya masharti yeyote.
Msemaji wa Polisi, Advera Senso alikiri kuhojiwa
kwa Kilewo akisema ni kawaida kwa jeshi hilo kumuita mtu na kumhoji kwa
mujibu wa taratibu na sheria zake.
0 comments:
Post a Comment