Marekani
leo inaadhimisha miaka 50 tangu kuuawa kwa kupigwa rais wa 35 wa nchi
hiyo, John F. Kennedy, mjini Dallas tarehe 22 Novemba mwaka 1963 akiwa
na umri wa miaka 46, na hivyo kuuzima mshumaa wa matumaini kwa wengi.
”Ich
bin ein Berliner,”hayo ni maneno aliyoyazungumza aliyekuwa rais wa
Marekani, John F. Kennedy, wakati wa hotuba yake aliyoitoa mjini Berlin,
Ujerumani wakati nchi hiyo ilipokuwa imegawanyika sehemu mbili, ya
Mashariki na Magharibi.
Hii
leo ikiwa inakumbukwa miaka 50 tangu kuuawa kwake, matukio kadhaa
yatafanyika ikiwemo kugonga kengele za Kanisani, kuweka mashada ya maua
kwenye kaburi lake, watoto kuimba nyimbo, bendera zitapepea nusu
mlingoti na kusoma hotuba zilizowahi kutolewa na Kennedy.
Wakazi wa Dallas kukusanyika Dealey Plaza
Maelfu
ya wakaazi wa Dallas watakusanyika kwenye eneo la Dealey Plaza, ambako
msafara wa Rais Kennedy ulipita wakati alipopigwa risasi na kuuawa
majira ya sita na nusu (12:30) mchana.
Akitoa
amri ya bendera kupepea nusu mlingoti hapo jana Alhamisi, Rais Barack
Obama aliuelezea utawala wa Kennedy uliokuwepo wakati wa utawala wa
mzozo wa makombora ya Cuba, wakati wa Vita Baridi na katika juhudi za
kutetea haki za Wamarekani weusi na wanawake wa Marekani. Rais Obama
amesema urithi wake hauna budi kukumbukwa siku zote.
Picha ya Lee Harvey Oswald, aliyemuuwa Kennedy, JF Kennedy
Sauti
ya Kennedy inaendelea kuwepo katika historia ya Wamarekani wengi na
hasa katika hotuba yake aliyoitoa siku alipoapishwa kuwa rais wa
Marekani Januari 20 mwaka 1961, aliposema, nanukuu ”Msiulize nchi yenu
itawafanyia nini, Uliza wewe utaifanyia nini nchi yako?”, mwisho wa
kunukuu.
Siku ya Jumatano Rais Obama alipongeza juhudi zote zilizofanywa na Kennedy, wakati akitoa nishani maalumu za uhuru za Rais.
Obama kukutana na wajumbe kadhaa Ikulu
Aidha,
katika kuadhimisha siku hii mjini Washington, Rais Obama atakutana
faragha na viongozi na wajumbe wa kujitolea wa kutoka kwenye mpango wa
watetezi wa amani ulioanzishwa kwa kumuenzi Kennedy, kwenye Ikulu ya
Marekani.
Huko
Boston maktaba ya John F. Kennedy itafunguliwa leo kwa ajili ya
kuonyesha picha na vifaa mbalimbali vilivyotumika wakati wa mazishi ya
kitaifa ya Kennedy ambazo hazijawahi kuonyeshwa hapo kabla.
Kennedy ni rais wa nne wa Marekani kuuawa akiwa madarakani, lakini mauaji yake ni ya kwanza kurekodiwa kwenye mkanda wa video.
Wengi
wanakataa kuamini kuwa mauaji hayo ni njama iliyofanywa na mtu mmoja
pekee mwanajeshi wa kikosi cha majini, Lee Harvey Oswald, aliyekuwa na
umri wa miaka 26 wakati huo, aliyeelekeza bunduki nje ya dirisha moja
kwenye chumba kilichokuwa ghorofa ya sita na kuufyatulia risasi msafara
wa rais.
Shule,
maeneo ya makumbusho, maktaba na makanisa kuzunguka Marekani, pia
yataadhimisha kumbukumbu hiyo, kwa kuonyesha mambo mbalimbali pamoja na
kutoa mihadhara.
Kennedy
atakumbukwa kwa kuwahamasisha watu kushiriki katika harakati za kijami
na watu wengi nchini Marekani bado wanao moyo huo. Nchini Ujerumani
kumbukumbu hiyo pia inaadhimishwa mjini Berlin.
0 comments:
Post a Comment