Hali ya kisiasa katika kambi ya upinzani nchini, imekuwa ya
kupanda na kushuka. Hii inatokana na migogoro inayoonekana kuvikumba
vyama vya upinzani hasa katika nyakati za kushika kasi kuelekea kwenye
mafanikio ya kweli.
Migogoro hii mingi huhitimishwa kwa kufukuzana na kusimamishana uanachama na mara nyingine kupelekana mahakamani.
Vyama vya NCCR-Mageuzi, CUF na TLP vina historia
hiyo. Matukio hayo yamevifanya vyama hivyo kuporomoka umaarufu wake,
heshima iliyojijengea katika jamii na hata nguvu.
NCCR-Mageuzi walipokuwa katika mgogoro
walihitimisha kwa kumfukuza na kumvua uanachama Mbunge wa Uvinza, David
Kafulila na mgogoro ndani ya CUF uliishia kumvua uanachama mbunge wake
wa Jimbo la Wawi, Hamad Rashid Mohamed. Wote hawa mashauri yao yapo
mahakamani.
Sasa ni zamu ya Chadema ambacho kimetangaza
kuwavua vyeo waliokuwa viongozi wake wa ngazi za juu, Zitto Kabwe,
ambaye amevuliwa nafasi ya Naibu Katibu Mkuu na ile ya Naibu wa Kambi
Rasmi ya Upinzani Bungeni pamoja na Dk. Kitila Mkumbo ambaye amevuliwa
nafasi ya Ujumbe wa kamati kuu.
Matukio hayo ya kufukuzana uanachama kwa vyama
hivyo vikubwa vya siasa, ndiyo yanayosababisha kuwepo kwa maswali
yanayokosa majibu kuhusu nafasi ya kambi ya upinzani nchini.
Maswali yanayokosa majibu ni endapo uamuzi huu
mgumu wa Chadema utasababisha kukijenga chama hicho au utakifanya chama
hicho kikuu cha upinzania nchini kufuata nyayo za CUF, NCCR-Mageuzi na
TLP na swali la pili ni iwapo hali hiyo ni kiashiria cha upinzani kukua
au kudidimia. Wasomi na wachambuzi wa masuala ya siasa pamoja na
wanasiasa wanajibu swali hili kama ifuatavyo.
Profesa Gaudence Mpangala
Msomi na mchambuzi wa masuala ya siasa nchini,
Profesa Gaudence Mpangala anasema uamuzi unaofanywa na vyama wa
kuwafukuza au kuwasimamisha viongozi wake unaweza kuwa halali kulingana
na sababu zilizosababisha kufikia uamuzi huo.
“Inaweza kuwa ni hatua halali kama waliosimamishwa
kweli walifanya mambo yanayohatarisha uhai wa chama,” anasema Profesa
Mpangala.
Anasema chama kama Chadema ni kikubwa kinachoweza
kushinda uchaguzi mkuu ujao, hivyo kinapaswa kuwa na viongozi
walioshikamana na kuwa na nia moja. Endapo kuna viongozi wanaoonekana
kwenda kinyume, chama kina haki ya kufanya uamuzi wa namna yoyote wenye
lengo la kukinusuru.
“Chadema ni chama kikubwa kinachoweza kushika
dola…kinahitaji mshikamano mkubwa kwa viongozi wake na kuhakikisha
hawatokei wasaliti….kama ni kweli waliosimamishwa ni wasaliti ni halali
kabisa,” anasema Profesa Mpangala.
Anaendelea “Nidhamu kwa wanachama na nidhamu kwa viongozi ni
kitu muhimu sana…kama viongozi hawana nidhamu ni rahisi sana chama
kusambaratika,” anasema.
Anaongeza kueleza kuwa ni lazima Chadema kiwe
imara ili kiweze kushika dola na hiyo itawezekana endapo viongozi
watakuwa na msimamo mmoja wa kukijenga chama na siyo kukisaliti.
Kuhusu endapo uamuzi huo unaweza kukidhoofisha
chama, Profesa Mpangala anasema, “Kama hizo tuhuma siyo za kweli
kinaweza kudhoofika (Chadema) maana viongozi hao wanao ushawishi mkubwa
kwa watu wanaokiunga mkono chama hicho, hivyo lolote linawezekana,”
anasema. Masuala ya usaliti ndani ya vyama vya siasa yapo duniani kote
na kwamba haishangazi kama hilo limetokea Chadema au ndani ya chama
chochote kingine.
Dk Charles Kitima
Aliyekuwa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha St.
Augustine (SAUT) Dk Charles Kitima, anasema bado kunaonekana kuwa na
pengo la demokrasia ndani ya vyama vya siasa nchini.
Anaendelea kuna pengo la uelewa wa demokrasia
ndani ya vyama vya siasa nchini, vyama vitambue kuwa demokrasia ni
kusahihishana na kujisahihisha.
Dk Kitima alisema kuwa na mitazamo tofauti siyo
usaliti ni demokrasia na kusema ni vyema busara zitumike katika
kutofautisha kati ya usaliti na mawazo tofauti ya wanachama na viongozi
pamoja na misimamo ya vyama.
Anasema hata hivyo endapo mtu au kiongozi anafanya
kitendo cha usaliti kinachoonekana pia ni kuvunja Katiba ya nchi huyo
moja kwa moja anakuwa mkosaji na ni sahihi kukabiliana naye.
“Wote wanaotuhumiwa na waliovuliwa vyeo ni wasomi
wazuri na sidhani kama nia yao ni kuhujumu… pengine wanayo nia ya
kujenga na viongozi wenzao wanapaswa wawe tayari kupokea
mabadiliko…wapokee mawazo ya kujengwa yanayoletwa ndani ya vyama vyao
hata kama ni mawazo yanayotumiwa na wapinzani wao,” alisema.
“Katika harakati za kujenga unaweza kukosea au
ukapatia...na kuwa na mtazamo tofauti siyo usaliti, nadhani demokrasia
iheshimiwe, hujuma zibainishwe na mahakama ndiyo iwe na mamlaka ya
kutamka hizi ni hujuma na huu ni usaliti na siyo mambo haya kutazamwa
juu juu” alisema Dk Kitima.
Hamad Rashid
Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohammed,
anasema matukio ya kufukuzana na kutuhumiana baina ya viongozi
yanayofanywa na watendaji wakuu wa vyama yatasababisha upinzani kudumaa.
Hamad anasema vyama vya siasa vimekuwa na usultani wa kuonekana
kuwa vinapaswa kuongozwa na baadhi ya watu huku wanachama wengine wenye
uwezo na mawazo mapya na yasiyopendwa na wakubwa wakitafutiwa mbinu ya
kuondolewa.
“Hili linalotokea Chadema sasa ni matokeo ya mfumo
mbovu wa uongozi ndani ya vyama vya siasa nchini….vingi haviongozwi
kama taasisi, tunahitaji vyama kukaa na kujengwa kama taasisi, viwe na
mfumo wa mabadiliko ya uongozi utakaosaidia vyama kukua” alisema
Alisema hali hii ikiachwa vyama vya upinzani
vitaendelea kudumaa na kubakia historia kwani wafuasi wao walio wengi
ambao ni vijana watavikimbia kutokana na kuona hawana nafasi ya kuleta
mabadiliko ndani ya vyama vya upinzani.
“Vijana wanakosa matumaini ya kushika madaraka
katika ngazi za juu ndani ya vyama vya upinzani…hawaoni matumaini ya
fursa ya kuongoza vyama hivi kutokana na mfumo wa uongozi
uliopo…viongozi waliopo wanaonekana hawataki challenge, hawataki watu
wenye uwezo nje ya wao.
Anasema ili demokrasia ikue viongozi wanapaswa
wakubali mawazo ya wengine na mtu mwenye mawazo tofauti asionekane kuwa
msaliti au mkosaji anayepaswa kuwekwa pembeni.
Hamad Rashid anaongeza kuwa hata wafuasi wa vyama
vya upinzani ambao wengi wao ni vijana wameanza kuvikimbia vyama vya
upinzani na kurejea CCM baada ya kukosa imani na vyama vya upinzani
ambavyo vinaonekana kutokukubaliana na mawazo mapya ya vijana.
0 comments:
Post a Comment