Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, wameshindwa
kupitisha Makadirio ya Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2014/2015 iliyokadiriwa
kukusanya Sh87 bilioni kutoka katika vyanzo mbalimbali vya mapato vya
halmashauri pamoja na ruzuku kutoka serikalini.
Baraza hilo lilitarajiwa kupitisha rasimu hiyo ya
bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2014/2015 zikiwa pamoja na ruzuku kutoka
Serikali Kuu na wahisani Sh77.2 bilioni matumizi ya halmashauri Sh9.1
bilioni pamoja na michango ya wananchi Sh239.3.
Akisoma bajeti hiyo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya
Jiji la Mwanza, Karsan Hida alisema kuwa fedha hizo zinatarajiwa
kukusanywa kutoka katika vyanzo vya mapato vya halmashauri pamoja na ada
mbalimbali.
Alisema kuwa kipaumbele walichoweka ni pamoja na
ujenzi wa Jengo la Wodi ya Wanaume katika Hospitali ya Wilaya ya
Nyamagana itakayogharimu Sh2 bilioni, ujenzi wa jengo la Mahakama ya
Jaji Sh2 bilioni.
Hida pia alisema kuwa halmashauri imelenga
kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo pamoja na utoaji wa huduma
kama Afya, Elimu, Kilimo na Mifugo, ushirika pamoja na maendeleo ya
jamii na sekta ya uvuvi katika halmashauri hiyo.
Wakichangia katika bajeti hiyo, Diwani wa Igoma
Adamu Chagulani alisema kuwa bajeti hiyo haijitoshelezi, kwani vyanzo
vingi vya mapato vimeachwa bila kutolewa ufafanuzi katika makabrasha
hali inayowapa wasiwasi madiwani kuijadili rasimu hiyo.
Walipendekeza bajeti hiyo kuandaliwa upya ili
ikidhi mahitaji ya wananchi wa Mwanza, huku wakiwataka kuangalia upya
miradi ambayo haijakamilika kuweza kuitengea bajeti.
“Kuna nyumba chache tu zinalipa kodi, wakati zingine zaidi ya 800 hazilipi kodi kama inavyotakiwa,” walisema madiwani hao.
Naye Mbunge wa Viti Maalumu wa Mkoa wa Mwanza,
Maria Hewa alisema kuwa kuna vyanzo vingi vya mapato kama shule za
binafsi hazitozwi kodi bila kutaja sababu husika.
“Mkurugenzi ufanye kazi na watumishi wako ili
tufike mahali tunapata mafanikio. Tumeungana vyama vyote, tunataka
bajeti irudi na ichambuliwe kwa upya na kuangalia vyanzo vyote vya
mapato,” alisema Hewa.
Akiahirisha kikao hicho, Meya wa Jiji la Mwanza,
Stanslaus Mabula alisema kuwa kilichofanyika ni kurekebisha matatizo
ambayo yataisaidia halmashauri ili kuweza kupata mafanikio.
0 comments:
Post a Comment