Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Kilimanjaro inawashikilia wahamiaji
haramu 57 raia wa Ethiopia kwa tuhuma za kuingia nchini kinyume cha
sheria.
Ofisa Uhamiaji, Johaness Msumule amekiri kukamatwa
kwa wahamiaji hao haramu na kusema, walikamatwa Januari 10 mwaka huu
saa saba usiku katika Kijiji cha Ghona Chekereni, wilayani Moshi mkoani
hapa. PICHA NA MAKTABA
Msumule alisema kukamatwa kwa wahamiaji hao haramu
kumetokana na taarifa ya watu wema, akiwamo Mwenyekiti wa Kijiji cha
Ghona, Ramadhan Abdallah aliyewataarifu kuwapo kwa watu hao kandokando
ya Barabara ya Moshi/Dar es Salaam wakisubiri usafiri.
“Tulipigiwa simu usiku wa manane na kuelezwa uwepo
wa wahamiaji haramu, na sisi tulichukua magari tukishirikiana na Jeshi
la Polisi na tulipofika tuliwakuta wakiwa chini ya ulinzi wa sungusungu
wa kijiji,” alisema Msumule.
Alisema wahamiaji hao haramu husafirishwa kwa
pikipiki kwa njia za panya na kufikishwa eneo la chekereni, ambalo ni
moja ya vituo vyao vikuu na baadaye kupakiwa kwenye malori kwa lengo la
kusafiri kwenda Dar es Salaam na baadaye kuelekea Afrika Kusini.
“Mara baada ya kuwakamata lilitokea Fuso kwa lengo
la kuwachukua, lakini walipowaona sungusungu gari hilo lilikimbia
sambamba na mtu aliyesadikiwa kuwa kinara wa kuwasafirisha wahamiaji,”
alisema
Alisema kutokana na maeneo ya Chekereni, Kifaru na
Makuyuni kuwa kitovu cha kuwahifadhi wahamiaji haramu,Ofisi ya Uhamiaji
imelenga kuweka doria ya usiku kwa kutumia askari na magari kuanzia
Januari 13 mwaka huu lengo likiwa ni kukamata vinara wanaowasafirisha na
kumaliza tatizo hilo.
0 comments:
Post a Comment