Waziri Kivuli wa Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi, Halima Mdee amemshukia Waziri wa wizara hiyo,
Profesa Anna Tibaijuka kwa kushindwa kutatua mgogoro wa shamba la
Kapunga mkoani Mbeya na badala yake ameukuza.
Kwa mujibu taarifa yake kwa vyombo vya habari
aliyotoa jana, Mdee alisisitiza kuwa ripoti zilizotolewa kwenye vyombo
vya habari wiki iliyopita zinathibitisha kukua kwa mgogoro huo hasa
baada ya wananchi kunung’unika mbele ya waziri huyo wakati wa ziara
yake. Mdee alisema kuwa hatua hiyo imeonyesha kuwa mgogoro huo wa Shamba
la Kapunga lililopo wilayani Mbarali, mkoani Mbeya umechukua sura mpya
kwa sasa kwa kuigharimu taswira ya kisiasa ya Waziri Profesa Tibaijuka
ambaye wananchi walimlaumu kutokana na kubadili msimamo juu ya suala
hilo.
“Taarifa zimeonyesha kwamba mgogoro huo bado
unatokota, tena safari hii ukionekana dhahiri kuigharimu Serikali ya CCM
kwa kuonyesha kuwa sera zake za kusimamia ardhi zimeshindwa na haiwezi
kuwajibika kwa ajili ya wananchi,” alisema Mdee, ambaye pia ni Mbunge wa
Kawe kupitia Chadema.
Mdee alisema iliripotiwa kuwa Profesa Tibaijuka
hakuwafurahisha wananchi wa Kapunga baada ya kuingia ndani ya gari la
mwekezaji ambaye ndiye yuko kwenye mgogoro na wananchi kugombania eneo
hilo, kisha aliposhuka akawa amebadili msimamo aliokuwa nao awali .
Alisema Waziri Tibaijuka alitakiwa kwenda Kapunga
huku akiujua ukweli wa chimbuko la mgogoro huo ni serikali yenyewe
kupitia Nafco ambayo iliuza ardhi kwa mwekezaji (hekta 7,370) na
kusajili na kupata hati kwa eneo lote ikiwamo hekta 1870 za kijiji.
0 comments:
Post a Comment