Moja ya sifa za mwanasiasa ni kuwa mvumilivu na kukubaliana na mabadiliko hata kama yatachelewesha kasi ya kutimiza ndoto yake.
Wiki iliyopita Kamati Kuu ya Chadema ilimtangaza
Grace Tendega kuwa ndiye atakayepeperusha bendera ya chama hicho
kuchuana na wagombea wa vyama vingine kuwania ubunge katika uchaguzi
mdogo wa Jimbo la Kalenga, mkoani Iringa.
Uchaguzi huo mdogo utakafanyika Machi 16, 2014
kuziba nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo
marehemu, Dk William Mgimwa aliyefariki dunia Januari 1, 2014 katika
Hospitali ya Mediclinic Kloff, Afrika Kusini alikokuwa akipata matibabu.
Uteuzi wa Tendega umetangazwa na Mwenyekiti wa
Chadema, Freeman Mbowe akisema kuwa kwa mujibu wa taratibu ndani ya
chama hicho, jina la mgombea hupitishwa na Kamati Kuu baada ya
kujiridhisha kuwa ametimiza vigezo vinavyotakiwa.
Kauli hiyo ‘ilitengua’ matokeo ya kura za maoni
zilizopigwa na wanachama wa Chadema wa jimbo hilo, na kumpa ushindi
Lucas Mwenda kwa kura 132 huku Tegenda akiibuka wa pili akiwa na kura
122.
Mbowe anasema kuwa matokeo ya kura za maoni
yaliyotangazwa awali hayakuwa na ‘baraka’ za Kamati Kuu, hivyo hayakuwa
rasmi, hivyo akawataka wapigakura wampokee mgombea aliyepitishwa na
chama.
Mbowe anaongeza kuwa: “Bwana Sinkala (Mwenda) bado
ni kijana mdogo, mwanasheria wetu na tunahitaji kumkuza zaidi, basi
vyombo vyote vimeshauri nafasi hii apewe mama Tendega kwa sababu ana
sifa za kutosha.”
Baadaye azizicompdoc.blogspot.com ilipata nafasi ya kuzungumza na
Mwenda, ambaye pia alihudhuria mkutano wa Mbowe na wanahabari jijini
Dar es Salaam, na wakati wote alionekana kuwa kimya huku akimsikiliza
kwa makini mwenyekiti wake.
Nilitaka kujua anajisikiaje baada ya Kamati Kuu
kumtangaza mgombea aliyekuwa ameshika nafasi ya pili, jambo ambalo lina
historia ya kuleta msuguano katika historia ya siasa za Tanzania.
Mwenda anasema: “Kama panya ameingia kwenye
kihenge (hifadhi ya chakula), hatuwezi kujali rangi ya paka kuondoa wale
panya. Sio lazima mimi niwe mbunge, akichaguliwa mtu yeyote mwenye
kutaka kuleta mabadiliko nitamkubali.
Anaongeza: “Kuteuliwa kwa mgombea mwingine
kutawashtua sana wapiga kura, lakini tutajitahidi kuwaambia Wanakalenga
kuwa shida yao siyo aina ya mtu bali ni mabadiliko.”
Mwenda anasema kuwa alifahamiana na Tendega wakati walipokuwa
wote kwenye Chama cha Jahazi Asilia, ambapo alimsaidia kuwania Jimbo la
Kalenga mwaka 2005 na kufanikiwa kuibuka namba mbili.
“Mabadiliko haya nimeyapokea kwa moyo mzuri kwa
sababu dada Grace ninamfahamu tumeanza kupambana naye tangu Jahazi
Asilia, nilimsapoti sana, akapotea kidogo mimi nikaendeleza mapambano,
amekuja tena Kamati Kuu imetumia vigezo vyake kumchagua,” anasema.
Anasema wananchi wa Kalenga wanahitaji mbunge atakayewaletea maendeleo
kwa sababu jimbo hilo linaongoza kwa umaskini mkoani Iringa.
“Wananchi wa Kalenga hawasomewi mapato na matumizi, hawajui hata kama fedha za ruzuku zimekuja kwenye vijiji vyao,” anasema.
Anasema kuwa tatizo kubwa lililopo Kalenga ni
mfumo mbovu wa kupeleka maendeleo kwa wananchi ambao unasimamiwa na CCM,
hatua iliyolifanya jimbo hilo kuongoza kwa umaskini katika Mkoa wa
Iringa.
“Kama tunahitaji mabadiliko hatuhitaji rangi ya
mtu, jinsi au kabila lake, tunachohitaji ni kuona maendeleo yanapatikana
baada ya kukosekana kwa miaka 52,” anasema Mwenda.
Ujasiri wa kupokea uamuzi wa Kamati Kuu ya chama
aliouonyesha Mwenda huenda ukasaidia kupingana na maneno aliyowahi
kusema mpigapicha maarufu wa Marekani, Mark Cohen, kwamba: “Hakuna
kinachoweza kumkwaza mpigakura zaidi ya kumbadilishia mshindi wake.”
Tendega, mwajiriwa wa Taasisi ya Elimu Tanzania
(TIE) tangu mwaka 2006 na msomi mwenye Shahada ya Uzamili katika sanaa
ya saikolojia ya jamii, anasema anaamini uteuzi wake utapokewa kwa
shangwe na wakazi wa Kalenga kwa kuwa wanaifahamu historia yake ya
utendaji kazi.
Tendega anasema chama chake kimethibitisha kukomaa
kidemokrasi kwa kufanya mambo yake kwa uwazi, ndiyo maana wagombea
wenzake wote 14 wameunga mkono uteuzi huo.
“Mgombea mwenzangu ameupokea uteuzi wangu kwa moyo
mweupe na ndiyo maana yupo hapa, kwa hiyo hakuna namna yoyote wagombea
kugawanyika katika hili,” alisema Tendega. Tendega ambaye amewahi kuwa
mjumbe wa nyumba kumi wa CCM katika Mtaa wa Kichangani, Kihesa, Iringa
Mjini kati ya mwaka 1996 hadi 1998, amewahi pia kufanya kazi katika
Wizara ya Kilimo na Chakula.
Akizungumza kwa simu kutoka Iringa kwa masharti ya
kutokutajwa jina ktk Blog kwa kuwa siyo msemaji wa Chadema, mmoja wa
viongozi wa chama hicho jimboni humo, anasema kuwa uamuzi uliofikiwa na
Kamati Kuu utaungwa mkono na wanachama wengi kwa kuwa Tendega ana nguvu
ya ushawishi ndani na nje ya chama.
“Hawa watu walitofautiana kura kumi tu, uamuzi
utakuwa uliochukuliwa utakuwa ni sahihi kwa sababu kwenye kura ya maoni
tuliangalia tu idadi ya kura, wakati wao wanataka sifa za ziada,”
anasema.
Tayari Chama cha Wananchi (CUF) kimeshatangaza kutomsimamisha mgombea katika uchaguzi huo, huku CCM kikimnadi Godfrey Mgimwa, mtoto wa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo.
Tayari Chama cha Wananchi (CUF) kimeshatangaza kutomsimamisha mgombea katika uchaguzi huo, huku CCM kikimnadi Godfrey Mgimwa, mtoto wa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo.
0 comments:
Post a Comment