Waziri
wa Ujenzi, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo alikuwa Mgeni
Rasmi katika hafla ya utiaji saini mikataba ya ujenzi wa barabara
itakayotekelezwa katika mikoa ya Ruvuma na Mtwara.
Miradi
hiyo itahusisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kati ya
Namtumbo na Tunduru ambayo imegawanywa katika sehemi tatu ambazo ni
Namtumbo – Kilimasera (km 68.20), Kilimasera – Matemanga (km 58.70) na
Matemanga-Tunduru (km 60.70).
Tayari
Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) ambayo inayofadhili ujenzi huo kwa
pamoja na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), imetoa kibali kwa ujenzi
wa sehemu mbili za kuanzia Namtumbo hadi Kilimasera na Matemanga hadi
Tunduru. Sehemu kati ya Matemanga na Kilimasera itasubiri kibali kutoka
Benki ya Maendeleo ya Afrika ambacho pia kinatarajiwa kutoka hivi
karibuni.
Hii
ni mara ya pili kwa sehemu hiyo ya barabara kupata makandarasi. Awali
kampuni ya Progressive-Higleig Joint Venture kutoka India ndiyo
iliyokuwa imeshinda zabuni hiyo mwaka 2010 lakini baadaye ikasimamishwa
kutokana na kushindwa kutimiza masharti ya kimkataba na kuonyesha
udhaifu katika utekelezaji wa mradi huo.
Katika
hatua nyingine kesho pia utasainiwa mkataba wa ujenzi wa sehemu ya
barabara inayoanzia Mangaka mkoani Mtwara hadi Nakapanya (km 70.50)
katika mkoa wa Ruvuma. Vile vile utasainiwa mradi mwingine wa ujenzi wa
barabara kwa kiwango cha lami kuanzia Nakapanya hadi Tunduru (km 66.50)
utakaotekelezwa mkoani Ruvuma.
Kusainiwa
kwa miradi hii ni faraja kubwa kwa wakazi wa mkoa wa Ruvuma pamoja na
mikoa yote ya kusini kwani barabara hiyo ni kichocheo kikubwa kwa
shughuli za kiuchumi na kijamii katika maeneo hayo.
Hafla
ya utiaji saini wa miradi hiyo imefanyika leo (Jumatatu) tarehe 17
Februari, 2013 katika Hoteli ya Court Yard (Protea) hapa jijini Dar es
Salaam kuanzia saa 3:00 asubuhi.
0 comments:
Post a Comment