Welcome to our online store Portal

Template Information

Thursday, March 27, 2014

HALI HALISI BUNGE LA KATIBA

http://azizicompdoc.blogspot.com/  “Uvumilivu una mwisho wake, ukifika wakati huo tutawaambia Watanzania nini kinachoendelea na sisi tunakusudia kufanya kitu gani.”PICHA|MAKTABA
Kuna njama. Maneno haya mawili ndiyo yametumiwa na pande mbili zinazopingana ndani ya Bunge Maalumu la Katiba, kuelezea hali iliyojitokeza jana wakati wa kikao cha Bunge hilo kuhusu mvutano wa mabadiliko ya kanuni.
Njama zinazoelezwa na pande hizo ni za kuvuruga mchakato wa Katiba Mpya, zikirejea yaliyotokea jana jioni ikiwamo zomeazomea hali iliyomlazimu Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta kuliahirisha Bunge hadi leo jioni.
Baada ya kuahirisha Bunge hilo, Sitta alikutana na waandishi wa habari na kusema kwamba kuna njama za baadhi ya wanasiasa kutumia vurugu kuhujumu mchakato wa upatikanaji wa Katiba, badala ya kujenga hoja.
Bila kuwataja wanasiasa hao, Sitta alisema ikiwa hawataki kuendelea na mchakato huo, basi waondoke na kuwaacha wenye nia njema.
“Wanasiasa hawa wamedhamiria kuvuruga mchakato wa Katiba, tuhuma ambazo tumetuhumiwa leo na Lissu (Tundu) ni uongo na uzushi, mimi sihusiki na kupeleka marekebisho ya kanuni kwenye Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge,” alisema Sitta.
Sitta alikuwa anajibu mchango wa mjumbe wa Bunge, Tundu Lissu alioutoa mapema kwenye kikao cha jioni, akipinga kilichoelezwa ni njama za kutaka kubadili kanuni kinyemela ili kumsaidia mwenyekiti kulidhibiti Bunge.
Sitta alisema kwa kuzingatia kanuni ya 59 (1), Kamati ya Uongozi ina mamlaka ya kupeleka marekebisho ya kanuni ili kuliwezesha Bunge kufanya kazi vizuri.
Alisema hoja kwamba haiwezekani kufanyika mabadiliko hata kabla ya kuanza kutumika kanuni, siyo ya msingi kwani kila kitu kinabadilika kutokana na mazingira yake.
“Kamati ya Uongozi ndiyo ilipeleka waraka wa mabadiliko ya kanuni kwa Kamati ya Kanuni na Haki kwa kuzingatia kanuni, lakini hata kabla ya kujadiliwa na kamati husika inaonekana kuna wajumbe ndiyo wameichukua na kuifikisha bungeni,” alisema Sitta.
Alisema kwa kiasi kikubwa marekebisho ambayo yangesomwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Pandu Ameir Kificho, yalilenga kutoa ufumbuzi wa kanuni ya 37 na 38 juu ya upigaji kura ama uwe wa wazi au siri.
Sitta alisema pamoja na hilo, kulikuwa na marekebisho ya msingi kama kuweka utaratibu mzuri wa majadiliano katika kamati pia kuweka utaratibu wa vikao vya Bunge kuanzia Jumatatu hadi Jumapili.
“Mengi ambayo alikuwa anayasema Lissu kama ni takataka hayakuwapo katika taarifa ya Kificho,” alisema Sitta.

Kauli ya Lissu
Lissu katika mchango wake alibainisha kile alichoeleza kama ‘njama’ za kuchakachua kanuni, akihoji inawezekanaje kasoro zikaanza kuonekana wakati kanuni hazijaanza kutumika.
Alisema kanuni zilipitishwa mapema mwezi huu na kiporo pekee kilikuwa ni ile ya 37 na 38 kuhusu upigaji kura.
“Tumeletewa jedwali la marekebisho ambalo linaonyesha kuna marekebisho katika kanuni ya 14 (1), 32, 33, 35 na zile za 37 na 38 pamoja na 58(1) (d) zingine ni 63 (1) na 64 na kufutwa kwa kanuni ya 85, jambo ambalo ni kinyume kabisa na kanuni zetu,” alisema Lissu.
Mbunge huyo wa Singida Mashariki, alisema utaratibu wa kurekebisha kanuni umeelezwa katika kifungu cha 87 (2) kwamba, mjumbe akiona kuna hitaji la kurekebisha kanuni awasilishe pendekezo kwa mwenyekiti wa Kamati ya Haki na Kanuni na iwapo Mwenyekiti akiona inafaa atawasilisha mapendekezo hayo bungeni.
“Kanuni hazina hata wiki tatu, hazijaanza kutumika tayari mmeanza kuzichakachua hivi, kasoro mmezipataje wakati bado hazijaanza kutumika,” alihoji.
Huku akionyesha marekebisho hayo, Lissu alisema: “Hizi ni takataka ambazo hatutakubali ziingizwe ndani ya mabadiliko.” Alisema Kamati ya Uongozi haina mamlaka yoyote juu ya kanuni za Bunge.
Lissu kushtakiwa
Sitta alisema kutokana na lugha alizotumia Lissu juu yake, anakusudia kumfikisha kwenye Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge. Alisema atatoa utetezi na wale ambao wanamtuhumu wataeleza ili ukweli ujulikane.
Alisema vurugu za jana jioni, zilipangwa hata kabla ya kuanza Bunge hilo, kwani hata wajumbe wanaotokana na Ukawa walisusia kutoa maoni katika Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge.
“Wajumbe wao hata kwenye kamati walikuwa hawazungumzi na wakati wanatoka walisikika wakisema wataendelea na mkakati wao wa kufanya vurugu,” alisema Sitta ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Dalili za kuvunjika kikao hicho zilionekana mapema baada ya wajumbe kuingia ukumbi kwani baadhi walikuwa kwenye makundi yaliyoashiria kujipanga kwa jambo lililokuwa mbele yao.
Kwa muda kidogo ukimya ulitawala bungeni baada ya Sitta kuzungumza, kisha ilisikika sauti ikiomba mwongozo.
Mwenyekiti alitoa nafasi kwa Lissu akitimiza ahadi yake aliyokuwa ameitoa asubuhi kabla ya kuahirisha Bunge hilo.
Mapema jana asubuhi, Sitta alikuwa ameahidi kuwa angetoa nafasi kwa miongozo hata kama ingekuwa 20 au 30 ili kila mtu aweze kupata kile alichokuwa akikihitaji.
Baada ya Lissu kueleza tuhuma zake, zomea zomea ilianza bungeni kiasi cha kuvuruga na kuondoa utulivu.
Waziri wa Sheria na Katiba wa Zanzibar, Abubakar Khamis Bakary baada ya kuruhusiwa alisema Bunge linaendeshwa na kanuni “haiwezekani huko aliko aandike mambo yake na kuyapeleka kwenye kamati halafu yaletwe bungeni, jambo hili haliwezi kukubalika.”
Alisema Bunge hilo ni lenye hadhi na heshima kubwa lakini kanuni kukiukwa kwa kanuni na sheria husika kunapunguza hadhi yake.
Kauli za wajumbe hao ziliungwa mkono na mjumbe mwenzao Ismail Jussa ambaye alisema waliopendekeza mabadiliko ya kanuni walikaa mafichoni kutekeleza azma hayo.
Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, akizungumza huku akikatishwa na makofi yaliyochanganyika na zomeazomea na yeye akielekeza maneno yake kwa kelele hizo alisikika akisema, “sijazoea kuzomewa” na wakati mwingine akisema “sijazoea kupigiwa makofi.”
Baada ya utulivu kukosekana, Sitta aliahirisha Bunge hilo ili kwanza wajadiliane kabla ya kuendelea.

Wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) wamesema wataendelea kupambana ndani ya Bunge Maalumu hadi ipatikane Katiba nzuri na watakuwa wa mwisho kujitoa katika mchakato huo.
Pia wamebainisha kuwa kukimbia au kujitoa katika mjadala huo ni sawa na kuwaachia CCM walio wengi kwenye Bunge Maalumu watunge Katiba wanayoitaka wenyewe na hivyo kuzima mawazo ya wananchi.
Mwenyekiti wa Ukawa, Freeman Mbowe alitoa msimamo huo jana katika mkutano na waandishi wa habari huku akiweka tahadhari kuwa “Uvumilivu una mwisho wake, ukifika wakati huo tutawaambia Watanzania nini kinachoendelea na sisi tunakusudia kufanya kitu gani.”
Imeandikwa na Mussa Juma, Habel Chidawali na Editha Majura
Mbowe ambaye ni kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, alisema kuna dalili zinavyoonyesha kuwa CCM hakina nia njema ya kuwafanya wananchi wapate Katiba nzuri.
“Hakuna mwendawazimu ambaye anaweza kufanikiwa kutugombanisha na kutusambaratisha, lazima katika jambo hili tutashinda na matakwa ya wananchi yatachukua nafasi ndani ya Katiba.”
Kwa upande wake James Mbatia alisema Ukawa haiwezi kwenda kinyume na wala haitakuwa tayari kuwasaliti wananchi katika yale ambayo waliyapendekeza kwenye rasimu.
Hotuba za JK, Warioba kutojadiliwa
Matarajio ya wajumbe wa Bunge Maalumu kujadili hotuba ya Rais Jakaya Kikwete na ile ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba yameyeyuka.
Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta alisema amechukua uamuzi huo baada ya majadiliano ya kina na kuonekana ni kama kutanguliza mjadala wa Rasimu ya Katiba kabla ya wakati wake.
“Kumbukeni waheshimiwa Rasimu ya Katiba tutaijadili kwa mpangilio wa sura mbili kama haitafanyika marekebisho ya kanuni hivyo, tukijadili hotuba hizi, wabunge watajadili mahala popote panapowahusu na hivyo itaharibu kabisa utaratibu wa kanuni,” alisema Sitta.
Awali, ilipangwa hotuba hizo kujadiliwa hasa kutokana na hoja mbalimbali za wajumbe kutaka kujadiliwa hutuba hiyo.
Miongoni mwa wajumbe walioomba kujadiliwa kwa hotuba hizo ni Julius Mtatiro ambaye pia aliomba kurejeshwa kwa Jaji Warioba kutoa ufafanuzi kuhusu masuala yaliyoibuliwa na Rais Kikwete.

Mjumbe mwingine Tundu Lissu aliwaeleza waandishi wa habari kuwa alikuwa anakusudia kumjibu neno kwa neno Rais Kikwete katika kila hoja kwani hotuba yake ilikuwa na upungufu.

Related Product :

0 comments:

Post a Comment

Why Shop on Bongo Online?

We make your shopping experience easy and exciting with our multiple payment options, amazing deals and unbeatable prices. You may pay on delivery or online with your Mobile Money. We fulfill your orders within the estimated time frame at your preferred location. We are committed to serving you, and your satisfaction is of utmost importance to us. Rest assured that for a wonderful shopping experience, Bongo Online Shop is the best place to be

About

Swissgear Smart Bag

468x60 Ads

HIDDEN CAMERA

Support : tzamaizing@gmail.com | Tzamaizing Template | +255 653 33 29 24
Copyright © 2015. AZIZI COMPUTER DOCTOR - All Rights Reserved
Template Created by Tzamaizing Published by Tzamaizing
Proudly powered by Bongo Online Shop