Ofisi za Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema), Mkoa wa Arusha zimenusurika kuteketea baada ya watu
wasiojulikana kuwasha moto katika moja ya vyumba vyake jana alfajiri.
Wakati hayo yakitokea, msuguano ndani ya chama
hicho umeendelea kushika kasi baada ya jana, Mwenyekiti wake Mkoa wa
Singida, Wilfred Kitundu kujiuzulu akipinga hatua ya Kamati Kuu kumvua
nyadhifa zake aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe.
Moto Arusha
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas
alisema jana kwamba walipata taarifa za kuungua kwa ofisi hizo zilizopo
eneo la Ngarenaro saa mbili asubuhi.
Katibu wa Chadema Mkoa wa Arusha, Aman Golugwa
alisema chumba cha kompyuta ambacho kina kumbukumbu za wanachama wote
Kanda ya Kaskazini kimeathirika.
“Hii ni hujuma dhidi ya Chadema; watu hawa
walipanda juu ya ukuta na kuingia ndani kupitia kwenye dari kisha
kuchoma moto ofisi,” alisema Golugwa.
Alisema vyumba viwili ndivyo, vimeungua kabisa na
kwa bahati nzuri moto ulishindwa kusambaa na kuzimika baada ya umeme
kuzimwa. Katibu wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Wilaya ya
Arusha, Happiness Chale ambaye aliwahi kushuhudia tukio hilo alisema,
mhudumu wa ofisi hiyo, Jenipha Mwacha alibaini moto huo baada ya
kusambaa na kufika katika maliwato. Alisema kwa kawaida ofisi hiyo
inalindwa na walinzi wa Red Brigade.
Polisi walifika mapema eneo hilo na kuweka uzio
ili kuzuia watu kuingia katika ofisi hizo pamoja na kuanza uchunguzi wa
tukio hilo.
Wakati polisi wakiwa katika ofisi hizo, viongozi
wa Chadema Mkoa na Wilaya ya Arusha walikuwa wakitoa maelezo polisi
kuhusiana na tukio hilo.
Mwenyekiti Singida
Huko Singida, Kitundu amejiuzulu nafasi hiyo jana huku akieleza kuwa chama hicho kinakiuka misingi ya demokrasia.
Uamuzi wa Kitundu umekuja siku nne tu, tangu
Mwenyekiti wa Chadema mkoani Lindi, Ally Chitanda naye kujiondoa katika
nafasi hiyo akieleza kuchoshwa na uamuzi wa kikanda na kikabila
unaoendelea ndani ya chama hicho.
Katika taarifa yake ya jana, Kitundu ambaye pia ni muasisi na
Chadema mkoani Singida, alisema: “Nimeamua kujiuzulu nafasi yangu ya
Uenyekiti wa Mkoa wa Singida, ambayo nimeitumikia kwa muda mrefu
kutokana na kukiukwa kwa demokrasia ya kweli ndani ya chama,” alisema na
kuongeza:
“Binafsi ni mtu wa kwanza kujiunga na Chadema hapa
Singida na mtu wa 300 kujiunga na chama hiki kitaifa. Hiyo ni heshima
kubwa kwangu na sipo tayari kuipoteza kwa kukubali kuwa sehemu ya
udhalilishaji huu wa demokrasia uliopitiliza.”
Alipinga hatua hiyo ya Kamati Kuu ya Chadema
akisema ni kinyume na mambo ambayo chama hicho kinayahubiri kwa umma...
“Si vyema nikaendelea kupingana na dhamira yangu inayonituma kuwa
mwanademokrasia wa kweli.”
Awali, akizungumza na waandishi wa habari mjini
Singida, Kitundu alisema baada ya kupata taarifa za Kamati Kuu kuwavua
uongozi Zitto na wenzake, alimtumia ujumbe mfupi wa maneno Mwenyekiti wa
Chadema, Freeman Mbowe akimweleza: “Uamuzi mliofanya ni sawa na mtu
kujenga nyumba ya tope wakati mvua kali ikinyesha.”
Alisema mwenyekiti wake hakuwahi kumjibu. Mbowe hakupatikana jana kujibu madai hayo kwani yuko nje ya nchi.
Alisema baada ya kufanya kikao na wenyeviti wa
Chadema katika wilaya za Mkoa wa Singida, wamefikia uamuzi wa kulaani,
kupinga na kukemea uamuzi Kamati Kuu ya chama aliyoyaita kuwa ni ya
kipuuzi yaliyojaa chuki, hofu na wasiwasi mwingi.
Hata hivyo, Katibu wa Chadema Mkoa wa Singida,
Patrick Msuta alikiri kupokea barua ya kujiuzulu kwa Kitundu na kusema:
“Kama alikuwa na tatizo, angekatia rufani suala hilo katika ngazi
husika.”
“Uamuzi wake ni kama kutengeneza mgogoro na katika
mgogoro una kujenga au kubomoa. Sasa uamuzi wake hauwezi kubomoa chama,
kwani Chadema kuna watu wazuri wenye uwezo wa kukijenga chama. Chadema
hakuna ilichopoteza kwa uamuzi wake.
“Alichokifanya ni kama ametumia demokrasia yake
kupinga uamuzi wa Kamati Kuu na ametekeleza... lakini juzi tu hapa, Rais
Jakaya Kikwete alisema kuwa mtu ambaye hawezi siasa aache, akae kando
akalime, mimi nadhani huyu anatekeleza kauli ya Rais,” alisema Msuta.
Msuta, baadaye alisema kuwa uongozi wa Chadema
mkoani humo hauhusiki na yaliyozungumzwa na Kitundu: “Huo ni uamuzi wake
yeye mwenyewe, hakuna anayehusika na uamuzi wake wa kujiuzulu nafasi ya
uenyekiti.”
Chadema Mwanza watoa tamko
Chilongozi aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa Chadema,
kimechoka kuchafuliwa na kundi la vijana ambao wamekuwa wakitumika kwa
madhumuni na malengo yasiyofahamika na sasa kitawashtaki mahakamani.
“Tuko katika maandalizi ya mapokezi ya viongozi
wetu kichama mkoani Mwanza na tunalaani kauli ya Robert Gwanchele
anayejiita Mwenyekiti wa Matawi ya Chadema Mkoa wa Mwanza ikiwazuia
viongozi wa juu wa chama hicho kutokanyaga Mwanza.
“Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara
ya 17 inatoa uhuru wa kila Mtanzania kutembea sehemu yoyote ya nchi
ilimradi havunji sheria za nchi na waliotoa tamko la kuwazuia viongozi
wao wamevunja sheria za nchi,” alisema Chilongozi.
Slaa aanzia Shinyanga leo
Dk Slaa, leo anaanza ziara ya kikazi mkoani Shinyanga ambako atakagua shughuli mbalimbali za maendeleo.
Ofisa Habari wa Chadema, Tumaini Makene alisema
jana kuwa Dk Slaa anatarajia kuanza ziara yake wilayani Kahama na kesho
yake ataendelea na ziara hiyo mkoani Kigoma.
Hatua hiyo, imekuja siku chache baada ya viongozi
wa Mkoa wa Kigoma kumtaka Katibu huyo kuahirishwa ziara hiyo kutokana na
sababu zilizodaiwa kuwa za kiusalama.
0 comments:
Post a Comment