Wakati Rais Jakaya Kikwete jana akiongoza mamia ya wakazi wa Mkoa wa Iringa na mikoa ya jirani kwenye mazishi ya aliyekuwa Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa, Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameahidi kuwa Serikali itatekeleza ahadi alizotoa jimboni kwake.
Dk Mgimwa, ambaye alikuwa Mbunge wa Kalenga,
alizikwa jana saa 10 jioni katika kijiji cha Magunga kilichoko Kata ya
Maboga mkoani Iringa.
Dk Mgimwa aliyefariki Januari mosi mwaka huu
nchini Afrika Kusini, kutokana na tatizo la figo, alizikwa katika shamba
la makaburi lililopo karibu na nyumbani kwa wazazi wake katika kijiji
hicho.
Akitoa ujumbe wa Serikali katika mazishi hayo,
Pinda alisema wataziangalia ahadi alizotoa marehemu na kuzifanyia kazi
zile ambazo hazijakamilika.
“Katika kumuenzi marehemu Mgimwa, sisi Serikali tunamuenzi kwa kutekeleza mema yote aliyotuachia,” aliongeza Pinda.
Pinda alisema Serikali imepoteza waziri aliyetegemewa katia wizara husika na taifa kwa jumla.
“Zimetolewa sifa nyingi zikimwelezea Waziri Mgimwa
juu ya uaminifu wake. Mimi nimesimama hapa kuthibitisha hilo, kwa muda
mfupi alioteuliwa amefanya kazi kwa uadilifu na weledi mkubwa na sisi
katika Serikali tukasema sasa wizara imempata waziri anayestahili,”
alisema Pinda.
“Kati ya Oktoba 4-15 sisi serikalini tulimtuma
Mgimwa aende Marekani akafanye kazi moja na ndipo ilipogundulika kuwa
alikuwa na tatizo lakini yeye alivumilia hadi kazi ilipoishi ndipo
akarudi na alipofika akasema ngoja aende Afrika Kusini akaangalie afya
yake,” alisema Pinda.
Kwa upande wake, mtoto wa marehemu Godfrey Mgimwa
ambaye alisimama kutoa shukrani kwa Serikali na wananchi waliofurika
katika mazishi hayo, aliiomba Serikali kutekeleza ahadi kadhaa
alizoziacha baba yake kama njia pekee ya kuwafariji wanafamilia na
wananchi wa Jimbo la Kalenga.
“Siku 10 kabla ya kufariki dunia, baba aliniambia
kuwa wakazi wa Jimbo la Kalenga ninawapenda sana katika kipindi hiki
ambacho hali yangu si ya kuridhisha ningependa niwapelekee mabati 1,200.
Ametutoka bila ya kutekeleza ahadi hiyo, watoto na wanafamilia tunaomba
Serikali kutekeleza ahadi hizo kama njia pekee ya kutufariji,” alisema
Godfrey.
Godfrey alitaja miradi minne ambayo baba yake
alimweleza kuwa alikuwa anataka kuwatekelezea wakazi wa jimbo hilo kuwa
ni pamoja na umeme, minara ya simu, uanzishaji wa ushirika wa kuweka na
kukopa na barabara.
Akitoa mahubiri yake katika ibada ya misa ya
mazishi ya marehemu Mgimwa, Msaidizi wa Makamu wa Askofu wa Kanisa
Katoliki, Jimbo la Iringa, Padri Julius Kingalawe, alisema taifa
limefikia hatua mbaya ya watu kutokuaminiana.
“Watu hawaaminiani, mtu akimwona mwenzake anakuwa na hofu ya
kama atamfanya nini kwani watu wamefikia hatua hata ya kufanyiana mambo
mabaya ili wapate nafasi ama fedha. Siku hizi hata katika vikao muhimu
kumekuwa na malumbano,” alisema Kingalawe.
Akizungumza kwa niaba ya Kiongozi wa Kambi ya
Upinzani Bungeni, Mchungaji Peter Msigwa alisema kifo cha Mgimwa ni
pengo kwa Serikali, jimbo lake na hata upinzani kwa kuwa alikuwa
kiongozi wa tofauti na wengine .“Sisi tunasema Mgimwa alikuwa kiongozi
mwadilifu, msikivu tena mchapakazi, upinzani tunasema ni pigo sababu
yeye amekuwa tofauti na viongozi wenzake wa kisiasa bungeni ambao
wanapotekeleza majukumu yao ya kisiasa wanaegemea katika itikadi za
chama chao,” alisema Msigwa ambaye ni Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema).
Ibada hiyo ya mazishi iliyoanza saa nne kamili,
ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Chama Cha Mapinduzi akiwamo
Makamu Mwenyekiti, Phillip Mangula na Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana.
Pia baadhi ya mawaziri na manaibu mawaziri na hata
Chifu wa Wahehe, Mtwa Mfwimi wa pili, Abdul Adamu Sapi, ambaye alisifia
utendaji wake wa kazi.
0 comments:
Post a Comment